18/02/2026
Meneja wa mgodi wa Jitegemee Holding upande wa nishati safi, ndugu Bosco Mabena, amewahimiza wananchi na wafanyabiashara kuchangamkia fursa zinazopatikana katika maeneo ya migodi ili kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa mkoa. Wito huo umeelekezwa kwa makundi yote, hususan vijana na wajasiriamali wadogo, ili waweze kutumia vizuri rasilimali zilizopo kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.
Mabena ametoa kauli hiyo wakati wa uwasilishaji wa mradi katika Baraza la Biashara la Mkoa wa Ruvuma, mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Songea Club uliopo Manispaa ya Songea. Amesema kuwa uwekezaji katika sekta ya madini umefungua milango kwa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika utoaji wa huduma na bidhaa zinazohitajika migodini.
Akizungumza katika mkutano huo, Mabena ameeleza kuwa licha ya kampuni yao kujihusisha na uchimbaji wa makaa ya mawe, pia wamezingatia utunzaji wa mazingira kwa kuongezea thamani rasilimali hiyo ili iweze kutumika k**a nishati safi majumbani. Amesisitiza kuwa wanaunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais za kulinda mazingira kwa kuhakikisha matumizi bora na salama ya makaa ya mawe.
Aidha, amefafanua kuwa nishati hiyo inaweza kutumika katika shughuli mbalimbali zikiwemo viwandani, taasisi za umma na matumizi ya majumbani, hatua itakayosaidia kupunguza gharama za nishati na utegemezi wa vyanzo visivyo rafiki kwa mazingira. Ameongeza kuwa mradi huo unalenga kuongeza ajira na kuinua kipato cha wananchi wa maeneo yanayozunguka mgodi.
Naye mfanyabiashara mdogo Rose Marry Amesema ushiriki wa wafanyabiashara wa ndani katika shughuli za mgodi utasaidia kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na kuchochea maendeleo ya mkoa wa Ruvuma kwa ujumla.