14/05/2026
Bweni la Wasichana Lateketea kwa Moto Kiteto, Mbunge Ole Lekaita Awatia Moyo Wanafunzi.
Mbunge wa Jimbo la Kiteto, Edward Ole Lekaita, amefika katika Shule ya Sekondari Engusero wilayani Kiteto kutoa pole kufuatia ajali ya moto iliyoteketeza bweni la wasichana shuleni hapo.
Mbunge huyo ametembelea eneo la tukio na kujionea madhara yaliyosababishwa na moto huo kabla ya kupata nafasi ya kuzungumza na wanafunzi pamoja na walimu kwa lengo la kuwapa faraja na kuwatia moyo baada ya kupatwa na janga hilo.
Akizungumza shuleni hapo, Wakili Ole Lekaita amesema jambo la muhimu zaidi ni kwamba hakuna madhara ya kibinadamu yaliyotokea licha ya moto huo kusababisha uharibifu wa bweni la wanafunzi.
“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwalinda watoto wetu katika janga hili. Kitu cha msingi ni kwamba watoto wetu wote wako salama,” alisema.
Aidha amewataka wanafunzi kuendelea kuwa na moyo wa subira huku akiwasisitiza kuendelea na masomo yao bila kukata tamaa kutokana na tukio hilo.
Mbunge huyo pia amewataka wananchi pamoja na wadau mbalimbali kuendelea kuwaombea wanafunzi hao ili waweze kuvuka kipindi hicho kigumu kwa utulivu na mshikamano.
Mpaka sasa chanzo cha moto huo bado hakijajulikana.