11/05/2026
DIT MWANZA YAFANYA MAFUNZO YA UWEZESHAJI WANAWAKE NA UONGOZI
Wanawake watumishi pamoja na wanafunzi wa k**e wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) Kampasi ya Mwanza wameshiriki semina ya siku mbili kuhusu uwezeshaji wanawake na masuala ya kijinsia (Women Empowerment in Leadership and Gender Workshop) yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kujitambua, kujiamini na kuimarisha uongozi binafsi.
Awali akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Mkurugenzi wa DIT Kampasi ya Mwanza, Dkt. Msumba, Mhandisi Issa Mwangosi ameishukuru taasisi ya Dr. Angela Daalmann pamoja na washirika wake kwa uamuzi wao wa kushirikiana na DIT katika kuwawezesha wanawake kupitia mafunzo yenye tija kwa maendeleo ya jamii na taasisi.
“Tunathamini mchango mkubwa wa Dr. Angela na washirika wake katika kuwawezesha wanawake wetu kupata maarifa ya uongozi, kujiamini na kujitambua.
Mafunzo haya yanaenda kuleta chachu mpya ya maendeleo kwa washiriki wetu na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Ujerumani,” amesema Mhandisi Mwangosi.
Mafunzo hayo yanawezeshwa na Dr. Angela Daalmann kutoka Ujerumani kupitia kampuni yake ya Anda GmbH, kwa udhamini wa Serikali ya Lower Saxony State ya Ujerumani kwa kushirikiana na DIT Mwanza.
Washiriki wa semina hiyo wanapata mafunzo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Gender Roles, Personal Leadership, Self-confidence, Positive Mindset, Thinking Straight pamoja na mbinu za kujitambua na kuthubutu katika kufikia malengo yao ya maisha na taaluma.
Aidha, mafunzo hayo yanapata ushirikiano kutoka kwa wasaidizi wa Dr. Angela ambao ni Khadija Ally kutoka STK Coaching pamoja na Yohana Misese kutoka Simiyu Sports Promotion Centre ya Bariadi.
Hatahivyo,Kupitia mafunzo hayo, DIT Mwanza inaendelea kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania na Ujerumani sambamba na kuunga mkono agenda ya maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa kuhusu uwezeshaji wanawake na usawa wa kijinsia.